Thursday, May 9, 2013

VIFAA TASWA-ZANZIBAR



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Kampuni ya Ocean Group of  Hotel ( OGH) ya Zanzibar ambayo inayomiliki  hoteli za kitalii za PEMBA MISALI SUNSET BEACH HOTEL,  AMANI BANGALOWS na ZANZIBAR OCEAN VIEW HOTEL, Ijumaa 10/05/2013  saa 7.00 mchana inatarajiwa kukabidhi vifaa vya michezo kwa timu ya mpira wa miguu ya CHAMA cha WAANDISHI wa HABARI za MICHEZO wa TANZANIA ZANZIBAR, TASWA-ZANZIBAR.

Makabidhiano hayo yanayotarajiwa kufanyika katika ukumbi wa mikutano wa hoteli ya Zanzibar Ocean View utaenda sambamba na kutiliana saini mkataba wa udhamini wa timu hiyo kati ya TASWA-ZANZIBAR na kampuni ya OGH ambao umelenga katika kuimarisha malengo ya chama hicho ya kuleta maendeleo ya michezo nchini.

Itakumbukwa kuwa toka kuzinduliwa kwa timu hiyo mwanzoni mwa mwezi Januari mwaka huu, imekuwa ni kiungo muhimu kati ya wanachama wa chama hicho na wadau wengine wa michezo wa ndani na nje ya Zanzibar.

Msaada na udhamini huo bila shaka utaongeza kasi ya wanachama katika kustawisha michezo nchini kupitia mpango wa chama hicho wa kufanya ziara maeneo mbali mbali kuhamasisha vijana kushiriki katika michezo.

Mkakati huo unaotambulika kama ‘OPERAESHENI SAKA VIPAJI’ ulioanza mwezi April mwaka huu kwa ziara ya kimichezo katika Wilaya ya Kaskazini ‘B’ Unguja ambapo timu hiyo ilicheza na mabingwa wa ligi daraja la vijana “central league”, itaendelea na ziara hiyo katika Wilaya ya Kaskazini ‘A’ siku ya Jumamosi wakati TASWA-ZANZIBAR  F. C itakapoumana na makamo bingwa wa ligi daraja la vijana wilayani humo timu ya DOGODOGO STARS.

Mchezo huo unatarajiwa kufanyika katika kiwanja cha skuli ya Mkwajuni ambapo mbali na mchezo huo waandishi hao watapata nafasi ya kutembelea ofisi za chama cha mpira wa miguu Wilaya ya Kaskazini ‘A’ na kupata nafasi ya kubadilishana mawazo na uzoefu na uongozi wa chama hicho.

TASWA-ZANZIBAR inaamini kuwa udhamini huu na ziara hizi zitasaidia kuibua vipaji vipya ili mamlaka husika na wadau wengine waweze kuviendeleza na bila shaka wadau wote hawatasita kutoa ushirikiano na misaada yao kila itakapohitjika.

Aidha TASWA-ZANZIBAR inaamini kuwa kwa pamoja tunaweza kusaidia maendeleo ya jamii yetu kupitia michezo kwani michezo mbali ya kuwa ni burudani, katika siku za karibuni imekuwa ni ajira ambalo soko lake ni pana linaloweza kuajiri watu wengi kwa wakati mmoja na kupunguza tatizo la ajira nchini. Basi tushirikiane, ‘kwa pamoja kidogo kidogo tutafika’.
Imetolewa na;       MWINYIMVUA A. NZUKWI
          Mwenyekiti, TASWA-ZANZIBAR
09/05/2013 – ZANZIBAR.

Monday, May 6, 2013

BALOZI SEIF AKUTANA NA UJUMBE WA KAMPUNI YA SHANRAF AND PARTNERS YA OMAN


·        SMZ YAFUNGUA MILANGO KWA KAMPUNI YA KIOMANI
·        YENEWE YAAHIDI KUWEKEZA KUKUZA UCHUMI WA NCHI NA WATU WAKE
Na. Mwinyimvua Nzukwi, Zanzibar
Kampuni ya Kimataifa ya Shanfar & Partners Co. L.L.C yenye Makao makuu yake Mjini Salala, Nchini Oman imeonyesha nia ya kutaka kuwekeza vitega uchumi vyake hapa Zanzibar.

Nia hiyo imekuja kufuatia Visiwa vya Zanzibar kubarikiwa kuwa na rasilmali kadhaa ambazo bado hazijatumika katika kusaidia kuendeleza uchumi wa Taifa sambamba na kuongeza vipato kwa wananchi.

Mwakilishi wa Kampuni hiyo Ali Omar Al–Sheikh akiuongoza ujumbe wa Viongozi watano wa Kampuni hiyo alieleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi katika ofisi za Makamo huyo Vuga, Mjini Zanzibar.
 Omar amesema ujumbe wake umeridhika na rasilmali kadhaa zilizomo ndani ya Visiwa vya Zanzibar baada ya kupata fursa ya kutembelea maeneo mbali mbali mijini na vijijini katika ziara hioyo.
Alifahamisha kwamba taasisi yake inaangalia maeneo inayoweza kuwekeza baada ya kufanya uchambuzi wa kina wakilenga zaidi katika sekta ya utalii ambayo tayari imefikia hatua kubwa baada ya serikali kujitahidi kuimarisha miundo mbinu inayochochea ukuaji wa haraka wa sekta hiyo.

“ Zanzibar tayari imeshafanikiwa vyema katika uwekezaji wa Hoteli za daraja linalokubalika Kimataifa, kinachohitajika kwa wakati huu ni namna gani wanaweza kushajiisha makampuni ya kitalii kuweza kuitumia zaidi fursa hiyo” alifafanua Omar.

Aliongeza kuwa “ Tumeliangalia hata zao la karafuu linalotegemewa kwa Uchumi wa Zanzibar ambalo pia linaweza kuimarishwa mauzo yake katika soko la Kimataifa kwa kutumiwa zaidi utaalamu wa kisasa” na kusisitiza kuwa kampuni yake yenye makao makuu yake nchini Oman na matawi katika nchi kadhaa duniani.

Naye Ofisa Mkuu wa Kampuni hiyo  S. Srihar alimueleza Balozi Seif kuwa  katika jitihada za kusaidia maendeleo ya Zanzibar Kampuni yao ina uwezo wa kuyashawishi mashirika na Makampuni ya Kimataifa ya watembezaji Watalii kulitumia soko la utalii la Zanzibar katika kutembeza wateja na wageni wao.

 Srihar alisema kufanikiwa kwa mpango huo kunaweza kutoa nafasi ya ajira kwa wazalendo waliowengi nchini hasa vijana wanaomaliza masomo yao.

Akitoa shukrani zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliueleza ujumbe huo kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar bado inaendelea na juhudi za kuimarisha miundo mbinu katika sekta mbali mbali za kiuchumi hapa nchini ili kuinua uchumi wan chi na watu wake.

Balozi Seif alisema kuwa uimarishaji wa kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Zanzibar ni miongoni mwa hatua hizo zilizolenga kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji. 

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliushauri Ujumbe huo kuitumia fursa hiyo ili kusaidia uchumi wa Zanzibar sambamba na kuimarisha uhusiano wa Kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Oman.

Kampuni ya Kimataifa ya Kibiashara ya Shanfar & Patners Co. L.L.C ya Salala Nchini Oman imekuwa na ubia wa kibiashara na zaidi ya Makampuni saba ya kimataifa katika nyanja za viwanda, usafiri wa anga, utalii, huduma za Umeme, ujenzi na uchapishaji duniani kote.

Thursday, May 2, 2013

MAWASILILIANO VIJIJINI YAIMARISHE SEKTA MTAMBUKA


Na: Mwinyimvua Nzukwi, Zanzibar
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amesema maendeleo ya haraka kwa mataifa machanga yatapatikana iwapo suala la matumizi ya mtandao wa kisasa wa mawasiliano ya habari na mawasiliano yatapewa msukumo unaostahiki.
Alisema mfumo huo unaweza kuunganisha na kurahisisha utekelezeji wa majukumu ya taasisi pia unaweza kutoa ajira zaidi maeneo katika maeneo ya vijijini ambayo huduma  za mawasiliano hazijafika au ziko katika kiwango hafifu.
Balozi Seif alisema hayo alipokuwa  akiifungua warsha kuhusu mawasiliano vijijini iliyoandaliwa na mfuko wa mawasiliano kwa wote wenye makao makuu yake Nchini Uholanzi inayofanyika katika ukumbi wa hoteli ya Melia iliyopo Pwani Mchangani Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Alizitaja sekta za kilimo, biashara na elimu kuwa ni miongoni mwa sekta za zinazopaswa kupewa kipau mbela na  kuendelezwa kwa kutumia mfumo huo ili kuleta tija inayostahiki
Balozi Seif alifahamisha kuwa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Mapinduzi ya Zanzibar zimeanza kuchukua hatua za kufuata mfumo huu ili kutengeneza mazingira bora yatakayowezesha kukuza uchumi wa taifa
Alielezea kuwa kutokana na warsha hiyo kufanyika nchini Tanzania ni vyema washiriki wakatumia fursa hiyo kikamilifu ambayo alidai  itasaidia kuunganisha nguvu za pamoja katika kukabiliana na changamoto zilizomo kwenye mfumo huo.
“ Tumeshuhudia Mataifa kama vile Chile, Uturuki na Malaysia yalivyopiga hatua kubwa na ya haraka katika kuimarisha uchumi wao baada ya kuamua kutumia mfumo huo wa mawasiliano “. Alisema Balozi Seif.
Aliwataka washiriki wa warsha hiyo kufikiria njia zitakazowezesha kuongezeka kwa watumiaji wa teknolojia ya kisasa na kuwafikia wananachi walio wengi hasa wale walioko vijijini mara watakaporejea katika Mataifa yao.
Aliongeza kuwa licha ya Zanzibar kutajwa kuwa imepiga hatua katika matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA),  bado Serikali inaendelea na mikakati ya kusimamia upatikanaji wa huduma hizo ziwafikie wananchi wote mijini na vijijini.
Mapema akimkaribisha balozi iddi, Katibu mkuu wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Florens Martin Turuka alisema lengo la warsha hiyo ni kujenga nguvu zitakazosaidia kufikisha mawasiliano sehemu zisizo na huduma hizo.
Dr. Turuka aliongeza kuwa mfumo huu mpya ambao unaanza kuelekezwa katika mataifa machanga unakusudia kuanzisha mpango maalum wa mafunzo maskulini kwa kutumia mtandao wa mawasiliano ya moja kwa moja kati ya sehemu moja hadi nyengine.
Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na utolewaji wa huduma za mawasiliano ambazo zitawahusisha baadhi ya wasimamizi waliojiandaa kutoa huduma hizo kwa kupatiwa ruzuku katika maeneo ya vijijini.
“ Tumefarajika kuona wataalamu wa mfuko wa mawasiliano kwa wote wameamua kuifanya warsha hii hapa Zanzibar, hii ni  kufuatia visiwa hivi kupiga hatua ya maendeleo katika matumizi ya mawasiliano ya simu za mkononi “ . Alisisitiza Dr. Turuka.
Warsha hiyo ya siku tano ni ya sita ambayo inashirikisha Mataifa 12 ya Bara la Afrika wakiwemo wawakilishi wa mataifa ya India, Malaysia na Marekani  nchi zinazotajwa kupiga hatua kubwa katika uvumbuzi na matumizi ya teknolojia ya mawasiliano imedhaminiwa na wa Mfuko wa mawasiliano kwa wote wa  Uholanzi.

Friday, March 15, 2013

KAMATI ZA MAAFA, SHEREHE ZAKUTANA ZANZIBAR


·          BALOZI SEIF AONGOZA VIKAO
·        Zapongezwa, wananchi watakiwa kufuatilia taarifa za hali ya hewa
Kamati ya sherehe na maadhimisho ya kitaifa Zanzibar
imekutana kutathmini maadhimisho ya sherehe za miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar zilizofanyika mwezi Januari mwaka huu katika ukumbi wa nyuma wa Jumba la Wananchi Forodhani Mjini Zanzibar.
Kikao hicho kilichokuwa  ya Mwenyekiti wake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kilipokea taarifa ya tathmini ya maadhimisho hayo toka kwa kaimu Katibu wa Sekriterieti ya Kamati hiyo ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Said Shaaban ambae alisema kamati zote zilitekeleza vyema majukumu waliyopangiwa.
Said aliwaeleza wajumbe hao kuwa licha ya ufanisi ulioshuhudiwa pia zipo changamoto zilizojichomoza ndani ya utekelezaji wa majukumu ya kamati hizo ambayo ni pamoja na ufinyu wa bajeti kulingana na shughuli zilivyopangwa na ushiriki mdogo wa maafisa wa serikali na masheha kwa dhana ya kuwa sio wahusika.
Alisema katika kufanikisha maadhimisho ya mwakani ambapo Zanzibar
itakuwa inatimiza nusu sekriterieti imependekeza kuvishikisha na kuvitumia ipasavyo vyombo vya habari hasa vya serikali ili kushajiisha umma kuelewa umuhimu wa kushiriki katika maadhimisho.
Aidha Mwenyekiti wa Kamati hiyo alizipongeza kamati zote kwa kufanikisha vyema sherehe hizo na kufahamisha kwamba zilifanikiwa kutokana na ushirikiano mzuri uliokuwepo baina ya viongozi na wafanyakazi wa taasisi za umma, binafsi na wananchi.
“Wakati tunafanya tathmini ya sherehe za miaka 49 ya Mapinduzi ya Zanzibar
tunapaswa kuanza safari kubwa ya sherehe hizi kutimia nusu karne hapo mwakani”. Alisema Balozi Seif.
Nao wajumbe wa kamati hiyo walishukuru ushirikiano waliopatiwa na serikali na kuazimia kukutana tena katika kipindi cha mwezi mmoja ujao ili kupanga mikakati ya maandalizi kwa ajili ya maadhimisho ya mwakani.
Mapema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alikiongoza kikao cha kamati ya Maafa Zanzibar kujadili namna ya taifa linavyoweza kujiandaa dhidi ya maafa au matatizo  yoyote yanayoweza kutokea katika kipindi hichi cha mvua za masika zilizokwishaanza.
Kikao hicho kilichojumuisha wajumbe wa kamati hiyo toka Unguja na Pemba kilifanyika katika ukumbi wa Ofisini kwa Makamu huyo wa Rais iliyopo Vuga Mjini Zanzibar.
Akiwasilisha taarifa juu ya mwelekeo wa mvua za masika katika kipindi cha kuanzia mwezi wa Machi hadi Mei, Mkurugenzi wa Idaya ya Maafa Zanzibar Ali Juma Hamad alisema kuwa pamoja matarajio ya mvua kuwa za wastani katika maeneo mengi, bado upo uwezekano wa kutokea miripuko ya magonjwa.
Hamad alisema taasisi zinazohusika na maafa zinapaswa kuchukuwa  hatua za tahadhari kufanya maandalizi ya kukabiliana na madhara yanayoweza  kusababishwa na mvua za masika.
Akizungumzia sekta ya kilimo na usalama wa chakula Hamad alisema maeneo mengi ya ukanda wa pwani ya kaskazini pamoja na Visiwa vya Zanzibar yanatarajiwa kuwa na unyevu unyevu wa kutosha wa udongo hali ambayo wakulima wanashauriwa  kuendelea na taratibu za kawaida za kilimo cha msimu huu wa mvua za masika.
Akikiahirisha Kikao hicho Balozi Iddi aliiagiza Idara hiyo kwa kushirikiana na wataalamu wa taasisi washirika kuandaa utaratibu mahsusi wa kutoa taarifa rasmi kwa wananchi kuanzia wiki ijayo ili kuisaidia jamii kuchukua tahadhari dhidi ya majanga yoyote yanayoweza kutokea katika mvua za masika.
Alisema serikali na wananchi wote wanapaswa kujitayarisha kukabiliana na majanga au maafa ili kuepusha madhara yatakayosababishwa na mvua za masika zilizoanza mapema mwezi huu.
Wakichangia wajumbe wa kamati hiyo walisema wananchi wengi  hadi sasa hawajawa na utamaduni ya  kufuatilia mienendo ya mifumo ya hali ya hewa nchini ambayo ni muhimu katika maisha yao ya kila siku licha ya taasisi zinazohusika na hali ya hewa kutoa taarifa hizo mara kwa mara.

Monday, February 18, 2013

ASKOFU MUSHI KUZIKWA KITOPE

ASKOFU MUSHI KUZIKWA JUMATANO

MAZISHI ya marehemu Askofu Veratus Gabriel Mushi wa kanisa katoliki jimbo la zanzibar aliyweuawa kwa kupigwa risasi jana asubuhi yanatarajia kufanyika Jumatano katika makaburi ya Kitope mkoa wa Kaskazini Unguja.

Akizungungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Shangani mjini Zanzibar, Askofu Mkuu wa Kanisa hilo jimbo la Zanzibar Agostino Shao alisema kanisa lake limepokea kwa mshtuko tukio hilo na kwamba linaendelea na maandalizi ya mazishi yanayotarajiwa kufanyika katika makaburi ya viongozi wa kanisa hilo katika kijiji cha Kitope, wilaya ya Kaskazini 'B', Unguja.

Alisema kanisa lake linafanya mawasiliano na ndugu wa marehemu ili kujua ni watu gani wataotaka kuhudhuria katika mazishi hayo pamoja na wageni.

"Tunachokifanya toka jana baada ya kukabidhiwa mwili wa marehemu majira ya saa kumi jioni ni kuratibu juu ya namna ya mazishi yatakavyokuwa pamoja na wageni tunaotarajia kuwapokea katika mazishi hayo", alisema Askofu Shao.

Pamoja na kuelezwa kuridhishwa kwake na hatua zilizochukuliwa na jeshi la polisi toka kutokea kwa tukio hilo, Askofu Shao alisema ipo haja kwa jeshi hilo kuhakikisha linawajibika ipasavyo ili kukomesha vitendo vya uhalifu si tu kwa viongozi wa dini na maeneo yao ya ibada bali pia kwa raia wote.

Akionesha kutoridhika na kutofanyiwa kazi kwa taarifa za kutokea kwa matukio mbali mbali dhidi ya kanisa na viongozi wake, askofu huyo alisema kuna haja maalum kwa Rais kufanya marekebisho ya uongozi wa jeshi hilo kwa upande wa Zanzibar ili lifanye kazi kwa kuzingatia sheria na kufanya juhudi katika kuzuia uhalifu kabla ya kutokea.

"Kuna taarifa nyingi tumekuwa tukitoa kwa jeshi la polisi lakni taarifa hizi zimekuwa hazifanyiwi kazi kikamilifu na kuwa ndio chanzo cha matukio mengi ya kihalifu ndani ya nchi", alisema Askofu Shao.


SMZ YATOA TAMKO

SERIKALI ITWASAKA WALIOMUUA ASKOFU MUSHI
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imewataka wananchi wa imani zote kutoa ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama ili kuviwezesha kufanya uchunguzi wa kifo cha Askofu  Varistus Gabriel Mushi kilichotokea jana asubuhi.

Akitoa taarifa ya serikali, Waziri wa nchi Afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais Muhammed Aboud Muhammed ofisini kwake Vuga, alisema serikali italiwezehsa jeshi la polisi na vyombo vyengine ulinzi na usalama ili kubaini chanzo cha matukio hayo yanayoonekana kushamiri siku hadi siku.

Abuod alisema katika wakati huu wa majonzi wananchi na waumini wa dini zote wanapaswa kutulia na kuviacha vyombo hivyo vifanye kazi zao kwa utaalamu na mafunzo yao.

"Serikali haiwezi kuacha matukio kama haya yaendelee kwani yanaibua hofu kwa jamii na kuathiri jina la nchi yetu na uchumi wetu kwa ujumla", alisema Aboud.

Aliongeza kuwa serikali ya Zanzibar inaunga mkono tamko lililotolewa na serikali ya muungano linalovitaka vyombo vya usalama vya ndani na nje ya nchi ili kubaini chanzo cha matukio hayo na kama kuna watu au kundi lolote linalofadhili matukio hayo.

Kuhusu suala la uwezekano wa kuzagaa kwa silaha, Aboud alisema hali hiyo inatokana na mazingira ya Zanzibar yanayowezesha kuwepo kwa bandari zisizo rasmi (bubu) jambo ambalo serikali inalifanyia kazi na kuwataka wananchi kutoa taarifa juu ya watu wanaowatilia shaka kuhusika na vitendo vya uhalifu.

Aidha aliwataka viongozi wa dini kuendelea kuhubiri amani , utulivu na kuvumiliana miongoni mwa waumini wao ili kuiepusha nchi na matatizo ya kijamii na kiuchumi.

"Kwa miaka mingi watu wa dini tofauti wamekuwa wakiishi pamoja kwa mafahamiano na mshikamano hivyo bado kila mmoja wetu anapaswa kutimiza wajibu wake ili kuendeleza mshikamano uliodumu kwa muda mrefu", aliongeza Aboud.

Askofu Mushi aliuawa kwa kupigwa risasi tatu kichwani asubuhi ya Jumapili wakati akienda kuendesha misa ya Jumapili katika kanisa la mtakatifu Theressa liliopo Beit el Ras nje kidogo ya mji wa Zanzibar ambalo ni sehemu ya kanisa Katholiki jimbo kuu la Zanzibar.






Monday, January 28, 2013

KUMRADHI

Wandugu wapendwa, poleni kwa kutopokea habari na matukio mapya kwa muda mrefu sasa.
Hii ilitokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wangu na kwamba najua mlivyosumbuka au kukosa huduma hii ya  habari kwa muda wote.
Natanguliza shukurani kwa uvumilivu wenu na kuwaomba radhi kwa usumbufu uliojitokeza.
Nategemea kuwa tutaendelea kuwa pamoja.
karibuni sana.