Tuesday, February 13, 2018

"MABARAZA YA WADI NA KAMATI ZA MASHAURIANO YATAPUNGUZA URASIMU, KUCHOCHEA KASI YA MAENDELEO YA JAMII" - WAZIRI KHERI



NA MWINYIMVUA NZUKWI
Imeelezwa kuwa kuanzishwa kwa mabaraza ya wadi na kamati kwa za mashauriano za shehia kutachochea kasi ya maendeleo, demokrasia na kupunguza urasimu katika utekelezaji wa shughuli za serikali.

Waziri wa nchi ofisi ya rais, tawala za mikoa, serikali za mitaa na idara maalum za SMZ Haji Omar Kheri ameeleza hayo katika mkutano na waandishi wa habari mjini Zanzibar akieleza kuwa kufanya hivyi pia ni utekelezaji wa katiba ya Zanzibar ya 1984.

Alisema katiba ya Zanzibar inatambua uwepo wa serikali za mitaa ambazo uchaguzi wa viongozi wake, madaraka na kazi zake zitakuwa kama zinavyoelekezwa na sheria za mamlaka ya serikali za mitaa namba 7 ya mwaka 2014.

Alisema kwa mujibu wa sheria hiyo serikali za mitaa zina ngazi mbili ambazo ni mabaraza ya manispaa au miji kwa maeneo ya mijini na halmashauri za wilaya katika maeneo ya vijijini.

Alisema mabaraza ya wadi na kamati za ushirikiano za shehia ni vyombo vya kiutendaji vitakavyokasimiwa madaraka ya kutoa huduma bora na endelevu kwa wananchi jkw kuzingatia misingi ya utawala bora.

“Misingi mikuu ya utawala bora ni pamoja na kuwepo kwa dhana ya ushirikishwaji, wa wananchi katika kubuni, kupanga na kutekeleza shughuli za maendeleo katika maeneo yao kwa kuzingatiwa uwazi na uwajibikaji”, alisema waziri Kheri.

Alisema ili kuyaweka mabaraza hayo kuwa na ufanisi ofisi yake imeandaa miongozo iliyozinduliwa Februari 13, 2018 ambayo inatoa taaluma kwa masheha na madiwani wote ambao kwa mujibu wa sheria wanapewa jukumu la kuwa viongozi wakuu wa vyombo hivyo.

“Ushiriki wa wananchi wote katika mabaraza haya ni haki ya kila mwananchi na hatutarajii wananachi kubabaishwa katika kupata haki yao hii kwa sababu yeyote ile isiyokubalika kwa kuwa miongozo hii imeandaliwa kwa lugha nyepesi kwa kila anaetaka ufafanuzi”, alisisitiza.

Aidha alieleza kuwa wizara yake itaendelea kutoa miongozo na elimu kwa watendaji mbali mbali watakaohusika katika uundwaji wa vyombo hivyo na kuwataka wananchi kushiriki kikamilifu katika michakato ya uundwaji wake.

Akizungumzia utekelezaji wa mpango wa ugatuzi wa madaraka ulioanza kutekelezwa mwezi Julai 1, 2017, waziri kheri alisema tathmini iliyofanywa imebainika kuwepo kwa mafanikio makubwa katika sekta zilizogatuliwa kutokana na kuwepo kwa usimamizi wa karibu ulioleta ufanisi.
“Kuna tofauti kubwa ya kiutekelezaji na kiusimamizi wa majukumu ya maafisa wa sekta zilizogatuliwa kutoka serikali kuu jambo ambalo linatupa moyo kuwa tuanaweza kuwa na ufanisi mkubwa katika maeneo mengine”, alisema.

Dhana ya ugatuzi wa madaraka kutoka serikali kuu kwenda katika serikali za mitaa Zanzibar imeanza katika sekta za afya ya msingi, elimu ya maandalizi na msingi pamoja na kilimo ambazo zipo chini ya usimamizi wa wakurugenzi wa manispaa na halmashauri za wilaya.


Kwa mujibu wa sheria namba 7/2014 ya serikali za mitaa vyombo hivyo vitaundwa na watu wa kada mbali mbali wanaoishi katika maeneo husika kwa ya kuteuliwa na wakuu wa wilaya baada ya kuomba nafasi hizo miongoni mwa watu wenye sifa za kitaaluma na kuheshimika na jamii husika.


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheri akifafanua jambo wakati alipokuwa akijibu maswali katika kutoka kwa Waandishi wa Habari baada ya kutoa taarifa kuhusiana na kuanzishwa Mabaraza ya Wadi na Kamati za Mashauriano za Shehia.



Mwandishi wa Habari wa kituo cha ITV - Zanzibar Farouk Karim akimuuliza maswali Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar Kheir mara baada ya kutoa taarifa kuhusu uanzishwaji wa  Mabaraza ya Wadi na Kamati za Mashauriano za Shehia katikas mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika katika Ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar Kikwajuni Mjini Zanzibar.


Afisa  wa Habari wa idara ya Habari Maelezo zanzibar Salum Vuai Issa akiuliza swali kutaka ufafanuzi juu ya taarifa ya uanzishwaji wa Mabaraza ya Wadi na Kamati za ushauri za shehia iliyotolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ Haji Omar Kheri.



Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa Serikali za Mitaa na Idara maalum za SMZ Haji Omar Kheir akizungumza na Waandishi wa Habari  kuhusiana na  kuanzishwa Mabaraza ya Wadi na Kamati za Mashauriano za Shehia.

No comments:

Post a Comment